Balozi Ombeni Yohana Sefue
Wasifu
Ombeni Yohana Sefue ni Balozi, mwanadiplomasia mwandamizi na Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu. Amewahi kuwa Katibu wa Baraza la Mawaziri, Katibu wa Baraza la Usalama la Taifa na Mkuu wa Utumishi wa Umma. Aidha, katika nafasi yake akiwa Katibu Mkuu Kiongozi alisimamia kazi za Tume na timu mbalimbali zilizoundwa na Rais wakati huo. Katika majukumu yake ya kidiplomasia, amewahi kuwa Balozi na mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, na Balozi wa Tanzania katika nchi za Marekani na Kanada. Amewahi pia kuwa mwenyekiti wa jopo la wataalamu kwa ajili ya kufanya Tathmini ya Masuala ya Utawala Bora barani Afrika (African Peer Review Mechanism).
Balozi Ombeni Yohana Sefue pia amewahi kuwa msaidizi wa Rais wa awamu ya pili Hayati Ali Hassan Mwinyi, na Rais wa awamu ya tatu Hayati Benjamin Willium Mkapa, na ndiye aliyesimamia uandishi wa vitabu vya marais hao ambavyo ni Maisha Yangu, Kusudi Langu cha Hayati Benjamin Willium Mkapa na Safari ya Maisha Yangu cha Hayati Ali Hassan Mwinyi. Vilevile Balozi Ombeni Sefue amekuwa Makamu Mwenyekiti wa Tume ya kuangalia jinsi ya Kuboresha Taasisi za Haki Jinai Nchini.